come

come
Tuletee habari za kijamii, michezo na burudani, email kabumbu1935@gmail.com

Simba, Yanga sasa shakani ‘Kagame Cup’

SERIKALI imesema hali ya usalama nchini Sudan katika jimbo la Darfur, siyo shwari na kushangazwa na uamuzi wa Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (Cecafa) kupeleka mashindano ya Kombe la Kagame nchini humo baadaye mwezi huu.
Cecafa ilitangaza mashindano hayo kufanyika nchini Sudan baada ya kuhakikishiwa na Serikali ya Khartoum uwepo wa usalama wa kutosha kwenye jimbo la Darfur, ambalo limekuwa kwenye mapigano kwa muda mrefu.
Katibu mkuu wa Cecafa, Nicholous Musonye alikaririwa akizitaka nchi zinazoshiriki kutokuwa na wasiwasi juu ya usalama wa nchi hiyo kwa sasa na kusisitiza usalama umeimarishwa sehemu zote.
“Tumehakikishiwa usalama na Serikali ya Sudan, kwa hiyo nchi zote zinazoshiriki zisiwe na wasiwasi katika hilo,” alikaririwa Musonye.
Akiongea bungeni jana jijini Dodoma, wakati wa majumuisho ya michango ya wabunge waliojadili makadirio ya matumizi ya bajeti ya wizara hiyo mwaka 2013/2014, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa,
Bernard Membe, alisema hakuna uhakika wa nchini Sudan.
“Wizara inachunguza na itatoa taarifa kuhusu hali ya usalama Sudan na kuna uwezekano mkubwa wa kuzuia ushiriki wa timu za Tanzania” alisema na kuongeza;
“Tutachunguza na inawezekana kabisa tukawataka wasiende katika mashindano hayo kwani uwepo wao nchini Sudan unaweza kuleta fedheha kwa taifa letu.”
Katika ufafanuzi wake Membe alishangazwa na uamuzi wa Cecafa kwa kuchagua mji wa Darfur kufanyika kwa mashindano hayo.
“Darful hakuna hoteli na hali ya usalama ni ya wasiwasi kweli na hata watu wanaokwenda huko wanapokewa na vikosi vya magari yasiyoingia risasi BPV (Bullet Proof Vehicles) na huvishwa nguo zisizoingia risasi,” alisema.
“Nimeshangaa mipango hii ya kupeleka wachezaji wa Tanzania bila kutafakari usalama wa vijana utakuwa katika hali gani, sijui kwa nini walichagua sehemu hii kufanyika mashindano haya.”
Tanzania inawakilishwa na Yanga kama bingwa mtetezi wa michuano hiyo na Simba kama bingwa wa bara msimu uliopita. Simba iko Kundi A na timu za El-Merrekh (Sudan), APR (Rwanda) na Elman (Somalia), wakati Yanga iko Kundi C sambamba na Express (Uganda), Ports (Djibout) na Vital’O (Burundi).