come

come
Tuletee habari za kijamii, michezo na burudani, email kabumbu1935@gmail.com

COASTAL UNION KUWATAMBULISHA BOBAN, NYOSSO KESHOKUTWA

Timu ya Coastal Union ya Tanga keshokutwa Jumatano itawatambulisha rasmi mbele ya mashabiki wachezaji wake wapya Haruna Moshi 'Boban' na Juma Nyoso (Pichani)  katika mechi ya kirafiki dhidi ya URA ya Uganda kwenye Uwanja wa Mkwakwani, Tanga.


URA ambayo juzi iliifunga Simba magoli 2-1 na jana kutoka sare ya 2-2 dhidi ya Yanga kwenye kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, inaondoka leo kwenda Tanga tayari kwa ajili ya mechi hiyo.

Akizungumza  jana, kocha wa Coastal Union, Hemed Moroco, alisema kuwa pamoja na mchezo huo kuwa sehemu yao ya maandalizi ya kwa ajili ya msimu ujao wa ligi kuu, pia watautumia kwa ajili ya kuwatambulisha nyota wao wapya wakiwamo wakongwe hao waliowasajili kutoka katika klabu ya Simba.

"Huu mchezo ni muhimu zaidi kwetu katika maandalizi, tumekuwa tukifanya mazoezi kwa muda sasa kwa hiyo URA watakuwa kipimo kizuri kwetu... na pia tutawatambulisha rasmi kwa mashabiki wachezaji wetu wapya... mashabiki wamekuwa wakisoma tu kwenye vyombo vya habari kuhusu usajili wetu lakini sasa watapata nafasi ya kuwaona wachezaji hao uwanjani," alisema Moroco.

Aidha, alisema kuwa watautumia mchezo huo kuangalia mapungufu ya timu yao katika kipindi hiki wanachojiandaa kwa ajili ya msimu mpya.

Aliwataka mashabiki wa soka mkoani humo kujitokeza kwa wingi kuwaangalia wachezaji wao na maandalizi yao kwa ajili ya msimu ujao wa ligi kuu unaotarajiwa kuanza Agosti 24 mwaka huu.

Kwa upande wake nahodha wa URA, Joseph Owino ambaye amewahi kuzichezea timu za Simba na Azam, alisema anaamini mechi dhidi ya Coastal Union itakuwa mzuri na yenye upinzani kwa kuwa amesikia mabadiliko ya timu hiyo.

Alisema kuwa ziara yao ya kuja nchini itawasaidia sana katika kukijenga upya kikosi chao ambacho kimesajili wachezaji wengi vijana.