come

come
Tuletee habari za kijamii, michezo na burudani, email kabumbu1935@gmail.com

Musonye: Acheni siasa, Simba Yanga ziende Darfur

BARAZA la Vyama vya Soka kwa nchi za Afrika Mashariki na Kati (Cecafa) limedai kwamba Darfur Kaskazini walikozipeleka Simba na Yanga kwenye Kombe la Kagame ni sehemu salama na kwamba madai ya kuwa hakuna amani ni siasa tu, lakini klabu hizo za Dar es Salaam zimejibu: "Aaah wapi hatuji."
Katibu Mkuu wa Cecafa, Nicholaus Musonye ameenda mbali zaidi kwa kusisitiza kwamba hawana mpango wa kubadilisha vituo vya Darfur kwavile mechi zote zitachezwa huko na hakuna mechi itakayochezwa mjini Khartoum.
Simba na Yanga ni miongoni mwa timu 13 zinazoshiriki Kombe la Kagame ambayo itachezwa kwenye miji ya Al Fashir na Kaduqli iliyoko Darfur Kaskazini ambako awali kulikuwa ngome za waasi na kumekuwa kukiripotiwa matukio kadhaa ya uvunjifu wa amani na usalama wa raia.
Musonye aliuambia mtandao huu jana Jumatatu kwamba; "Haya mambo mengine muache siasa, hiyo miji yote ina amani kabisa na nilishawaandikia Simba na Yanga pamoja na timu zote zinazishiriki kwamba usalama upo wa kutosha kabisa."
"Mimi nimelala kule siku tatu na wala sikupata usumbufu wowote, kuna amani kabisa. Na hoteli tulizowaweka Simba na Yanga ni za hali ya juu sana acheni siasa, timu zote zitakuwa kwenye hiyo miji wala hakuna mabadiliko yoyote tutakayofanya, acheni siasa,"alisisitiza Musonye akikanusha tamko la Waziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania, Bernard Membe alilotoa Bungeni Jumamosi kwamba Darfur si sehemu salama.