come

come
Tuletee habari za kijamii, michezo na burudani, email kabumbu1935@gmail.com

NYOSSO, REDONDO WAITUNISHIA MSULI SIMBA


 


Dar es Salaam. Juma Nyoso na Ramadhan Chombo wameutaka uongozi wa Simba kuwalipa kwanza haki zao kabla ya kufikiria uamuzi wa kuwatoa kwa mkopo kwenda klabu nyingine.

Katikati ya wiki hii, Simba ilitangaza kuwatoa kwa mkopo kwenda klabu ya Ashanti iliyopanda daraja msimu huu, lakini hatua hiyo pia ikifuata baada ya awali kusimamishwa kwa muda usiojulikana kwa utovu wa nidhamu.
Wachezaji wamesema hawako tayari kuondoka Simba kabla ya kulipwa malimbikizo yao ya mishahara na haki zingine walizostahili kupata kama wachezaji wa Simba.
Wamesema ndani ya klabu hiyo, hakuna anayewajali wala kuwasaidia kupata haki zao, hivyo wanakusudia kuandika barua Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kueleza malalamiko yao.
Akizungumza na gazeti hili jana, Nyoso alisema ameshangazwa na utaratibu wa Simba kumtoa kwa mkopo wakati klabu hiyo ikifahamu fika kwamba haijamlipa mishahara yake. Nyoso alisema wanachofanya viongozi wa Simba ni kuwaburuta na kuwanyima haki zao za msingi na hawako tayari kuona hilo linatendeka.
“Binafsi siendi Ashanti. Nataka wamalize kunilipa madeni yangu yote na kisha mimi ndiyo nitaamua wapi niende lakini siyo kwa kupangiwa na klabu ya Simba,” alisema Nyoso.
“Sioni taabu kukatisha mkataba wangu. Sijaona utaratibu wa kumtoa mchezaji kwa mkopo wakati anadai mishahara yake. Nimeamua kwenda TFF kuwashtaki,” aliongeza.
Aidha, Nyoso aliongeza kuwa viongozi wa klabu hiyo wamekuwa wakipigiwa simu na kushindwa kujibu na walipojaribu kwenda ofisini viongozi hao wamekuwa wakirushiana mpira kila mara.
Nyoso, Maftah na Chombo wamesema wanaidai klabu hiyo mishahara ya miezi miwili, na kwamba baadhi ambao hawakuwa wamelipwa walilipwa pesa zao baada ya kudai sana.
Gazeti hili lilimtafuta katibu mkuu wa klabu hiyo ambaye ndiye mwenye dhamana ya malipo kwa wachezaji lakini simu yake ilikuwa ikiita bila majibu.
Kwa upande wa Ofisa Habari wa klabu hiyo, Ezekiel Kamwaga alisema ni vyema wachezaji hao wakawa na subira ili walipwe fedha hizo kwa vile mwamuzi wa mwisho ni uongozi wa klabu.
Wakati huohuo, kiungo wa Yanga, Nizar Khalifan yupo katika mazungumzo na uongozi wa klabu ili kumwongezea mkataba mwingine baada ya kuridhika na kiwango alichoonyesha msimu uliopita.