
Kocha wa timu ya soka ya taifa ya Tanzania (Taifa
Stars), Mdenmark Kim Poulsen, kesho ataanika kikosi chake cha mechi ya
marudiano dhidi ya timu ya taifa ya Morocco (Simba wa Atlas)
itakayochezwa Juni 8 jijini Marrakech, Morocco katika kuwania kufuzu
kushiriki fainali zijazo za Kombe la Dunia zitakazofanika Brazil 2014.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Boniface Wambura alisema kuwa Poulsen atazungumza na waandishi wa habari kesho kwenye ofisi za makao makuu ya shirikisho hilo kuhusu mipango ya benchi lake la ufundi na kutaja kikosi cha Stars kitakachowavaa mabingwa hao wa Afrika wa mwaka 1976.
Katika mechi ya kwanza iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam Machi 24, Stars ilishinda 3-1, shukrani kwa magoli mawili ya Mbwana Samatta na moja la Thomas Ulimwengu.
Mbali na Morocco na Stars, timu nyingine za Kundi C ni Ivory Coast na Gambia. Mabingwa wa Afrika wa mwaka 1992, Ivory Coast
wanaongoza kundi hilo wakiwa na pointi 7, moja zaidi ya Tanzania iliyo katika nafasi ya pili, na tano mbele ya Morocco wanaoshikilia nafasi ya tatu huku Gambia wakiwa mkiani na pointi yao moja. Timu zote zimeshacheza mechi tatu za awali.