YANGA imeamua kusuka kikosi chake cha Ligi ya Mabingwa Afrika 
kwa kuanzia na nchi mbili zilizoko kwenye tano bora ya Afrika kwenye 
viwango vya Fifa na itaingia kambini rasmi Julai 3 ikipiga kambi ya wiki
 mbili jijini Mwanza ambako kuna uwanja mzuri wa CCM Kirumba.
Mabingwa hao wa Tanzania wamekabidhiwa majina matatu na wakala waliyempa kazi ya kuwatafutia wachezaji wa kigeni.
Mastraika wawili ni kutoka Nigeria ambayo ni ya 
nne Afrika na 31 duniani na mwingine ni wa Ghana iliyoko nafasi ya pili 
Afrika na ya 21 duniani kulingana na viwango vipya vya Fifa vilivyotoka 
mwezi huu.  
Mwenyekiti wa Usajili wa Yanga, Abdallah Bin Kleb 
licha ya kutotaja majina ya wachezaji hao kwa madai kuwa bado 
hawajafikia muafaka, alisema wamepewa masharti na matakwa ya wachezaji 
hao na kwamba wanajadiliana kabla ya kupata muafaka wa jina mmoja.
Bin Kleb alisema lengo lao kubwa ni kupata straika
 mwenye nguvu, machachari, umri mdogo, akili ya kufunga na mpambanaji 
kama ilivyokuwa kwa Mzambia Davies Mwape ambaye aliachwa msimu uliopita 
kutokana na umri.
Kiongozi huyo mwenye ushawishi mkubwa ndani ya 
Yanga alisema wamepania kusajili mchezaji kwa kuangalia ubora wa nchi 
yake na wako tayari kumlipa ilimradi ajue kutumbukiza langoni.
“Hatutamtangaza mchezaji,  tunataka kufanya kama 
ilivyokuwa kwa Haruna Niyonzima na Mrisho Ngassa ambao walitambulishwa 
wakiwa tayari wamesaini mkataba na klabu yetu, tupo makini sana katika 
suala hili,” alisema Bin Kleb.
“Unajua madhara yake, unaweza kuharibu mikakati 
yako ya kumpata mchezaji huyo, sisi tuna wakala siku hizi ambaye 
anafanya kazi hiyo kama klabu za Ulaya, wakala wetu akikamilisha 
mazungumzo na kukubali ofa yetu, tutasaini mkataba na kuweka mambo 
hadharani kama ilivyokuwa kwa wachezaji wengine,” alisema.
Alisema kuwa wachezaji hao ni wazuri na 
wanalingana kwa viwango vyao, ila jambo ambalo limewafuraisha ni jinsi 
walivyokuwa wapambanaji uwanjani na hasa katika kufunga mabao.
“Tunataka mabeki wakitoka uwanjani wawe 
wanasimulia wenyewe kuwa wamekumbana na  straika mwenye kila kitu au 
akitoka mapumziko asiwe na hamu ya kurejea tena uwanjani kipindi cha 
pili, huu ndiyo mkakati wetu kwa sasa na tunataka timu ya Ligi ya 
Mabingwa Afrika na wala si vinginevyo,” alisema.
Alisema Yanga itaondoka Julai 3 kwenda Mwanza kwa ajili ya kambi na mechi za mazoezi na watakaa huko kwa muda wa wiki mbili.
Kama Yanga, itampata straika huyo ina maana kuwa 
kati ya Yaw Berko au Kabange Twite itabidi aondolewe katika orodha ya 
wachezaji wa kigeni ili kubakiwa na watano tu.
 
 
