come

come
Tuletee habari za kijamii, michezo na burudani, email kabumbu1935@gmail.com

SERIKALI YAMFANYIA UPASUAJI MCHEZAJI WA ZAMANI WA YANGAi

SHUJAA wa Taifa na nahodha wa zamani wa Pan Africa, Yanga  na Taifa Stars, Jellah Mtagwa amefanyiwa upasuaji kutokana na tatizo la ugonjwa wa ngiri-maji, uliokuwa unamsumbua.
Nyota huyo wa zamani amefanyiwa upasuaji huo kwa gharama za serikali baada ya Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Michezo, Leonard Thadeo kufika nyumbani kwa mchezaji huyo.
Hatua hiyo ya serikali imechangiwa na mfululizo wa makala zilizoandikwa katika safu ya Mkongwe kwenye gazeti hili makala iliyoelezea maisha duni na maradhi ya kiharusi yaliyosababisha kupooza mkono na mguu wa kushoto wa mchezaji huyo.
Habari za nyota huyo zilisababisha Mbunge wa Kinondoni, Iddi Azzan kuhoji iwapo serikali ina mpango wowote wa kuwasaidia mashujaa wa zamani katika michezo akiwamo Mtagwa, mchezaji pekee nchini ambaye picha yake ilitumika katika stempu zilizochapishwa mwaka 1982.
Thadeo alikiri kufika nyumbani kwa Mtagwa kumjulia hali lakini alikataa kuzungumzia kwa undani kwa madai kuwa suala la nyota huyo lilishatolewa ufafanuzi na Waziri wa Habari, Vijana Utamaduni na Michezo wakati wa kuhitimisha bajeti ya wizara hiyo hivi karibuni katika vikao vya Bunge.
Akizungumza nyumbani kwake jana Jumatatu, Mtagwa alisema kuwa alifanyiwa upasuaji katika Hospitali ya Aga Khan baada ya kufuatwa na viongozi wa idara ya michezo.
“Alikuja Thadeo kuiwakilisha serikali na waliwezesha kufanyiwa upasuaji na Jumatano (kesho) naenda kutoa nyuzi,” alisema Mtagwa na kuongeza kuwa upasuaji huo umefanikiwa baada ya madaktari kumpima na kuthibitisha kuwa kiwango cha msukumo wa damu kimeshuka.
Mtagwa alisema licha ya ukosefu wa fedha uliosababisha ashindwe kufanyiwa upasuaji mapema lakini pia kiwango chake cha msukumo wa damu kilichosababisha apooze mkono wa kushoto na mguu mara nyingi ilikuwa juu hivyo kuwafanya madaktari kuahirisha upasuaji huo mara kwa mara.
“Kuna wakati kabla serikali haijajitokeza kuna watu walitaka kunisaidia lakini presha ilikuwa tatizo,” alisema na kuongeza kuwa anaendelea vizuri baada ya upasuaji na anaamini kuwa akiendelea kupata matibabu stahiki afya yake itaimarika.