come

come
Tuletee habari za kijamii, michezo na burudani, email kabumbu1935@gmail.com

Yanga yafunga mjadala wa Ngassa

Katibu Mkuu wa klabu ya Yanga, Lawrance Mwalusako, amesema klabu yake imefunga mjadala wa uhamisho wa mchezaji Mrisho Ngasa na sasa inasubiri maamuzi ya shirikisho la soka, TFF.

Akizungumza jijini Dar es Salaam, Mwalusako alisema kuwa Yanga haitishiki na madai ya uongozi wa Simba kuwa mchezaji huyo bado ni wao kwa kuwa Yanga imemsajili Ngassa kwa njia sahihi na haina shaka ya kutomtumia msimu ujao.
“Yanga ina viongozi makini na tunafanya kazi kisasa, hili suala la Ngassa kwetu tayari tumelifunga na tunasubiri kuanza kumtumia kwenye michezo mbalimbali," alisema Mwalusako na kueleza zaidi, "haya maneno mengine ni ya mkosaji tu. Hutuyaogopi.”
Kauli ya Mwalusako inafuatia kiongozi mmoja wa Simba kudai wiki hii hawatamruhusu Ngassa kuchezea Yanga bila kulipwa sh. milioni 25 kama fidia ya kuvunjwa kwa mkataba wanaodai kuingia naye; ambao ungeanza kufanya kazi mara baada ya mkopo wake kumalizika.
Lakini Mwalusako alisema Yanga ilikuwa na uhakika mchezaji huyo hajasaini timu yoyote kwa ajili ya msimu ujao bali alikuwa Simba kwa mkataba wa mwaka mmoja wa mkopo akitokea Azam.
Mchezaji huyo alimaliza mkataba huo mwishoni mwa msimu wa ligi kuu hivyo Yanga ilikuwa sahihi kumsajili, alisema Mwalusako.
“Hayo maneno mengine yanayosemwa nje sisi hatuna la kuongea, sisi tunafuata kanuni za usajili zinasemaje.
"Kamati husika ya usajili ya TFF itaamua na kutoa maamuzi lakini hatuoni cha kuamuliwa kwa sababu kila kitu kipo sawa.”
Mwalusako allisema mchezaji huyo ataanza kuitumikia Yanga mwezi ujao kwenye mashindano ya Kombe la Kagame la klabu bingwa ya Afrika Mashariki na Kati nchini Sudan.