come

come
Tuletee habari za kijamii, michezo na burudani, email kabumbu1935@gmail.com

ZIARA YA OBAMA YALETA NEEMA BONGO

Rais Jakaya KIkwete akisalimiana na Rais wa Marekani, Barack Obama katika Ikulu ya White House nchini Marekani. Akiwa nchini Rais Obama atafanya mazungumzo na Kikwete kisha watafanya mazungumzo ya pamoja na waandishi wa habari.

Ukitaka kumfahamu mtu, tazama aina ya watu wanaomzunguka. Msemo huu unaweza kutumika kuielezea Tanzania hasa baada ya kupata fursa ya kutembelewa na marais watatu wa taifa lenye nguvu zaidi duniani, Marekani.
Kwa mara ya kwanza, Tanzania ilitembelewa na Rais wa Marekani aliyeko madarakani, George W Bush mwanzoni mwa 2008 na sasa nchi imepata fursa tena ya kutembelewa na rais mwingine wa nchi hiyo, Barack Obama ambaye atakuwa ameambatana tena na Bush, jambo ambalo ni la kihistoria katika Bara la Afrika.
Pamoja na kwamba kuna hali ya kutoridhika na hali halisi ya nchi, kiuchumi, kisiasa na kijamii kutoka kwa baadhi ya Watanzania, hali inaonekana kuwa ni tofauti kabisa kwa Marekani ambayo mtazamo wake wa masuala ya nchi za nje unawakilisha mtazamo wa mataifa mengi ya magharibi.
Akizungumzia sababu za ziara hiyo kwa njia ya conference call kutoka Washington, Naibu Mshauri wa Masuala ya Ulinzi wa Ikulu ya Marekani, Gayle Smith alisema Obama anazuru Tanzania kwa sababu nchi hiyo ni rafiki mkuu wa Marekani katika Afrika Mashariki na kwamba imebobea katika misingi ya kidemokrasia.
Smith alisema Bara la Afrika hususan Tanzania ni moja ya masoko muhimu sana yanayoibukia ulimwenguni na Marekani ni lazima iongeze harakati zake barani humo.
“Kuna fursa nyingi za kiuchumi, biashara na uwekezaji jambo ambalo linaitisha umuhimu wa kampuni na biashara za Marekani kujikita zaidi Afrika,” anasema Smith.
Tofauti na ziara ya Bush ambayo ililenga zaidi kuisaidia Tanzania kutoa huduma bora kwa watu wake hususan afya; ziara ya Obama imetokana na maombi na msukumo kutoka kwa wafanyabiashara wa Marekani ambao waliitaka Serikali yao kuunda mikakati ya makusudi ya kuhakikisha nchi hiyo inakuza na kuboresha uhusiano wa kibiashara na Waafrika.
Wakati wa ziara ya George W Bush, Tanzania ilinufaika na msaada wa dola 698 milioni kwa ajili ya ununuzi wa vyandarua na dawa za kuulia mbu pamoja na kuendeleza mapambano dhidi ya Ukimwi.
Maambukizi ya Ukimwi yalianza kushuka mwaka 2008 kutoka asilimia saba mwaka 2003 hadi kufikia asilimia tano na mwaka huu.
Idadi ya watu ambao wanajitokeza kupimwa Ukimwi na kuchukua majibu yao imeongezeka kutoka asilimia 20 ya wanawake mwaka 2008 hadi kufikia asilimia 30 mwaka 2012 na kwa wanaume imepanda kutoka asilimia 19 mwaka huohuo na kufikia asilimia 27 mwaka 2012.
Kwa upande wa malaria, kaya tisa kati ya 10 zinatumia vyandarua vyenye dawa ongezeko ambalo ni mara nne zaidi ya idadi ya kaya zilizotumia vyandarua hivyo mwaka 2004.
Hali kadhalika, zaidi ya asilimia 70 ya watoto ambao wako hatarini kuambukizwa malaria walilala ndani ya vyandarua ongezeko ambalo pia ni mara nne zaidi ya idadi ya mwaka 2004.