come

come
Tuletee habari za kijamii, michezo na burudani, email kabumbu1935@gmail.com

RAGE AKINUKISHA SIMBA



 Mwenyekiti wa Simba, Aden Rage jana alitoka nje ya Ukumbi wa Bwalo la Maofisa wa Polisi, Oyesterbay chini ya ulinzi mkali baada ya kumalizika kwa mkutano wa klabu hiyo, ambao wanachama walishindwa kujadili kwa kina ajenda kutokana na vurugu na zomeazoea.


Kabla hata ya kufanyika mkutano huo, tayari kulikuwa na makundi ya wanachama wakiupinga na ndiyo hao ambao walitumia fursa ya kushiriki kwao kwenye mkutano kumzomea Mwenyekiti Aden Rage.
Mwenyekiti Rage alijikuta kwenye wakati mgumu kutokana na baadhi ya wanachama kumzomea wakati akiwasomea maelezo ya mikakati na maendeleo ya klabu hiyo, ingawa mwishoni alifanikiwa kuwatuliza baadhi ya waliompinga.
Kasheshe ya kuzomea-zomea iliendelea hata baada ya kuitwa mbele Mkuu wa Chuo Kikuu Huria, Tolly Mbwete kuzindua mpango mkakati wa maendeleo ya klabu hiyo.
Wakati Mbwete (Profesa) akisoma maelezo ya mkakati huo, baadhi ya mashabiki walisikika wakisema; “Hatutaki...hatutaki...toka, hatutaki kusikia habari ya Chuo Kikuu, tunataka matokeo mazuri uwanjani huo mkakati wenu hautusaidii.”
Pamoja na kuzomewa, Rage alimtaka Mbwete kuendelea kusoma maelezo ya mkakati huo huku kelele zikiongezeka kutoka kwa wanachama wengi, hali iliyowafanya wengine kushindwa kusikiliza kilichokuwa kikiongelewa.
Kama mwendelezo wa kupinga kilichokuwa kikiongelewa, baadhi ya wanachama waliondoka kwenye mkutano huo uliokuwa chini ya ulinzi wa askari zaidi ya 70.
Baada ya mambo kwenda vibaya, Rage aliwataka polisi kuwakamata wanachama waliokuwa wakifanya fujo ikiwa ni pamoja na kuwatishia kuwafuta uwanachama, jambo lililoibua zogo zaidi.
“Hatoki mtu hapa...tupo tayari kufa lakini hapa hatoki mtu...unatuburuza, hatukutaki...tumekuchoka ondoka,” wanachama walipaza sauti.
Mkutano huo, uliofunguliwa saa 3 asubuhi na kuhudhuriwa na wanachama 712 kati ya 1516 ambao ni hai, na wanachama hao walishindwa kuchangia kikamilifu ajenda hali iliyopelekea mambo mengi kupitishwa kienyeji.
Kwenye Uwanja wa Taifa Dar es Salaam, Simba ilipata kipigo cha mabao 2-1 katika mchezo wa kirafiki wa kimataifa dhidi ya timu ya URA kutoka Uganda.
Simba walikuwa wa kwanza kufunga bao katika dakika ya saba likifungwa na Betram Mombeki. URA walisawazisha kupitia kwa Lutimba Yayo dakika 60, na kisha akafunga bao la ushindi dakika ya 76.