come

come
Tuletee habari za kijamii, michezo na burudani, email kabumbu1935@gmail.com

JESHI LA WATU 25 LAKAMILIKA JANGWANI

YANGA imeweka wazi jeshi lake la wanaume 25 watakaotetea heshima ya timu hiyo msimu ujao kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika na Ligi Kuu Bara huku Kamati ya Usajili ikisisitiza kuwa inakamilisha usajili wa straika mmoja matata wa kigeni.
Katika orodha hiyo Yanga imewapiga chini wachezaji wazoefu waliokuwa kwenye safu ya ulinzi wakiongozwa na nahodha Shadrack Nsajigwa huku wengine wenye mkataba wakitolewa kwa mkopo kwenye timu zilizopanda daraja msimu huu.
Habari za uhakika ambazo mtandao huu  imezipata kutoka ndani ya Kamati ya Usajili zimebainisha kuwa wachezaji ambao kamati imeafikiana watemwe ni Shadrack Nsajigwa (ambaye atapewa majukumu kwenye benchi la ufundi),  Nurdin Bakari, Yaw Berko, Godfrey Taita, Shamte Ali, Rashid Gumbo, Stephano Mwasyika, Idrisa Rashid na kipa  Said Mohamed ingawa Hamis Kiiza bado suala lake limewekwa pembeni kwa muda.
“Tunafanya makubaliano na straika mmoja wa kigeni lakini ikishindikana tutabaki na Kiiza,”alisema kigogo mmoja wa kamati hiyo na kutaja watakaotolewa kwa mkopo kuwa ni  Ibrahim Job (anatafutiwa timu), Ladislaus Mbogo (Rhino ya Tabora), Omega Seme (Tanzania Prisons),  Rehani Kibingu na John Banda (Ashanti United).
Kwa mujibu wa kiongozi huyo ni kwamba kikosi kipya kitakuwa na wachezaji 25 tu wanne kati yao wakiwa wa kigeni.  Makipa: Ali Mustafa, Deo Munishi na Yusuph Abdul.
Mabeki wa kulia ni Mbuyu Twite na Juma Abdul huku kushoto wakisimama David Luhende na Oscar Joshua na mabeki wa kati ni Nadir Haroub, Kelvin Yondani na Rajab Zahir.
Viungo ni Athuman Idd, Frank Domayo, Haruna Niyonzima, Simon Msuva, Salum Telela, Reliants Lusajo,  Nizar Khalfan na mastraika ni Didier Kavumbagu, Jerryson Tegete, Mrisho Ngassa, Shaaban Kondo na Hussein Javu.
Orodha ya sasa ambayo Kabumbu Spoti  imeishuhudia inaonyesha kikosi kina wachezaji 22 lakini kiongozi huyo amesisitiza kwamba watatu waliosalia mmoja ni straika huyo wa kigeni ambaye amedai kwamba atatoka kwenye nchi moja ya Afrika ya Magharibi na wengine wawili watachaguliwa kwenye timu ya vijana ya Yanga.
Mwanaspoti ilimtafuta bosi wa usajili wa Yanga ambaye licha ya kutotaka kuweka bayana majina alisisitiza kwa kifupi kwamba; “Kwa sasa hatusajili tena wachezaji wa ndani, macho yetu yapo kwa mchezaji mmoja kutoka nje ya nchi ambaye tutamtangaza muda si mrefu. Tumefikisha asilimia 99 ya usajili tunasubiri hatma ya straika mmoja tu ambaye anatoka nje ya nchi,” alisema Abdalla Bin Kleb.
Bin Kleb alikiri kwamba uwezekano wa Kiiza na Kabange Twite kuendelea kuwemo Yanga itategemea na huruma na mipango ya Kocha Ernest Brandts ambaye anawasili leo Jumanne kutoka Uholanzi alikokuwa likizo.