come

come
Tuletee habari za kijamii, michezo na burudani, email kabumbu1935@gmail.com

MAKALA: YUSUF MANJI ANAVYOTUMIA FEDHA KUTAKA KUINUNUA FURAHA.

Na Fikiri Salum


BADO wanadamu wanajidanganya na starehe za Dunia, Dunia imejaa vitu vingi vya kuvutia lakini kinachomnyima usingizi mwanadamu ni Furaha ya Moyo wake.

Masikini licha ya kufurahia watoto wengi alionao lakini anashindwa kupata faraha kutokana na umaskini wake unaomsumbua, Anaamini akiwa na Fedha anaweza kuinunua Furaha anajidanganya.

Tajiri naye anaamini fedha zake anaweza kuinunua Furaha, Roman Abramovich bilionea wa kirusi aliyeinunua Chelsea kwa fedha nyingi bado anashindwa kufurahi licha ya kutumia mamilioni kadhaa kuwanunua kila aina ya wachezaji bora na kocha mwenye ujuzi mkubwa.

Wanadamu wanaendelea kujidanganya, Wanajua furaha inanunuliwa kama nguo dukani, furaha kama roho haionekani wala hainunuliwi unaweza ukawa na fedha lukuki lakini ukakosa furaha kwa kukosa watoto au kupata ulemavu wa viungo.


Hadithi hii inamuelezea mwenyekiti wa mabingwa wa soka nchini Yanga, Yusuf Manji ambaye ndie mmiliki wa kampuni ya Quality Group Ltd.

Manji ni mmoja kati ya matajili 10 hapa nchini wanaotikisa Alianza kuifadhili timu hiyo miaka ya hivi karibuni na alifanya kazi kubwa kuwaunganisha Yanga-kampuni na Yanga- Asili waliokuwa wakilumbana kwa muda mrefu.

Mgogoro wao ulipelekea kuyumba kwa timu hiyo na kusababisha kugeuzwa mteja na hasimu wake Simba kwa miaka mitano mfululizo, Kuyumba uko kwa yanga kulisababishwa na mgogoro huo, umeifanya Simba kumtambia Yanga hadi sasa, Manji alitumia fedha zake kumaliza mgogoro huo kweli fedha inaweza kutatua matatizo sio kununua furaha.

Manji aliwapatanisha viongozi wote wa pande zilizokuwa zikilumbana ambazo ni Yanga–Kampuni iliyokuwa chini yake Francis Kifukwe na Yanga asili ya mzee Yusuf Mzimba.

Manji aliifanya Yanga iwe moja na hatimaye aliweza kuisaidia na baadae kutamba kwenye soka la nchi hii kipigo cha mabao 5-0 dhidi ya hasimu wake Simba kilimuudhi milionea huyo na baadaye akaamua kugombea uenyekiti.

Nilishangaa sana kusikia milionea kama Manji anagombania uenyekiti kwenye klabu ya Yanga ambayo inamilikiwa na wanachama hasa wenye sifa ya kutimua viongozi mara kwa mara.

Kama imetokea bahati mbaya timu imefungwa na mahasimu wake basi viongozi waliopo madarakani kupata wakati mgumu kama si kupinduliwa, wakati Yanga imelala 5-0 na Simba timu hiyo ilikuwa chini ya mwanasheria Lyoid Nchunga.

Lakini alitimuliwa na baadaye kufanyika uchaguzi mdogo alio muweka Manji madarakani, lakini hivi karibuni alitangaza kuto gombea tena nafasi hiyo, nini kimemkuta hadi asigombee?

Manji aliingia Yanga kwa lengo la kutaka kuinunua furaha ndani ya moyo wake, alitaka timu yake ilipize kisasi cha kufungwa 5-0 na Simba, alipoona hafanikiwi akaja na mbinu ya kuwachukuwa wachezaji Nyota wote waliokuwa Simba walioisaidia ipate ushindi wa 5-0 dhidi yao.

Kwanza alitamani kuifunga Simba mabao mengi katika mzunguko wa kwanza wa ligi kuu bara, alitumia fedha yingi kuipeleka Yanga Pemba ili ushindi upatikane.

Ndege tatu za kukodi zilitosha kuisafirisha Yanga kutoka Pemba kuja Dar es Salaam. tayali kuivaa Simba, Yanga ilijiamini kabisa na kuonyesha kandanda safi nakuongoza 3-0 dhidi ya Simba katika kipindi cha kwanza, matokeo hayo yalisababisha mashabiki wa Simba kuzimia.

Manji alisimama jukwaani huku akionyesha vidole vitano kuwaambia Simba lazima apigwe 5, aliamini anaweza kuinunua furaha alitumia fedha nyingi kusajili wachezaji wenye majina makubwa kwenye ukanda huu wa Afrika mashariki.

Pia aliweza kuibomoa Simba, Manji alisajili nyota wa Simba kama Mrisho Ngassa, Ally Mustapha 'Barthez', Kelvini Yondani, Deogratus Munishi 'Dida', Athuman Idd 'Chuji' na wengineo.

Hivyo fedha za Manji zilikuwa tayali kuleta furaha, Simba ina matajiri wengi lakini hawakuwa tayari kutumbukiza mamilioni yao sababu kubwa hawaendani na mwenyekiti wa klabu hiyo Alhaj Ismail Aden Rage.

Hivvyo Simba ilikuwa kama yatima au mtoto wa masikini lakini katika kipindi cha pili waliweza kushangaza wengi baada ya kucheza soka zuri na kusawazisha mabao yote matatu.

Wanayanga waliumia sana kiasi kwamba walimchukia kipa wao Ally Mustapha `Barthez`, tangia mchezo huo hajacheza tena kikosi cha kwanza cha timu hiyo.

Hapo ndipo Manji alipocharuka na kutaka kuendeleza mikakati yake ya kuirudisha furaha, Alianza kuwaliza Simba nje ya uwanja baada ya kumsajili aliyekuwa kipa wake Juma Kaseja ambaye alikuwa mbioni kurejea tena msimbazi.

Pia alimchukua kiungo wa Ruvu Shooting Hassani Dilunga ambaye naye tayari alikuwa anatua Msimbazi pigo kubwa ambalo adi sasa linawaumiza Simba ni usajili wa Emmanuel Okwi.

Wanasimba wanalumbana na mwenyekiti wao kisa Okwi wanadai Rage alimuuza Okwi Tunisia bila ya kupewa chochote na baadae kushangaa anatua Yanga kiuraini.

Okwi alitua uwanja wa ndege na kupokewa na mashabiki lukuki wa Yanga walifurika kumlaki huku wakiwadhihaki mahasimu wao Simba usajili wa Okwi ulizua utata hasa timu hizo mbili zikiwa zinaeleka katika mechi ya kirafiki iliyofahamika kama Nani mtani Jembe.

Mechi hiyo iliandaliwa na wadhamini wakuu wa vilabu hivyo vikongwe kampuni ya kutengeneza bia ya TBL kupitia bia yake ya Kilimanjaro.

Yanga iliamini ujio wa Okwi, Dilunga na Kaseja unaweza kukomboa kipigo cha goli 5-0 waliingia uwanjani na matumaini kibao huku mashabiki wake wakiwa wamevalia jezi ya zenye jina la Okwi ambazo zilitolewa siku chache kabla ya kuwasili kwa mshambuliaji huyo nchini.

Fedha haikuweza kununua furaha, Yanga iliyotumia mamilioni ya Fedha ilijikuta inapigwa mabao 3-1 na Simba isiyo na uwezo wa kusajili mchezaji kwa milioni 40.

Siku chache tu baada ya Yanga kupokea kipigo cha mabao 3-1, Uongozi wa Yanga chini ya Yusufu Manji uliamua kusitisha mkataba wa makocha wake wote pia ikimsimamisha Nyota wake Athumani Idd 'Chuji'.

Uongozi unasema makocha wamechangia kipigo na timu kushindwa kucheza kandanda la kueleweka hivyo imechangia hata kujitoa Mapinduzi Cup.

Hata hivyo Yanga imekwenda Uturuki kujiandaa na michuano ya kimataifa pamoja na mzunguko wa pili wa ligi kuu Tanzania bara inayotarajia kuanza mwishoni mwa mwezi huu.

Kikubwa hapa nilicho kiona kwa Yusuf Manji ambaye ndio bosi wake anaamini furaha inaweza kununuliwa lakini ukweli uliopo kwamba furaha haiwezi kununuliwa kama nguo.

Unaweza kuoa mwanamke mzuri tena kwa bashasha lakini asikupende, ndiyo ilivyo furaha ya moyoni, Yenyewe imeumbwa na mwenyezi mungu lakini haionekani kwa umbo kwa kifupi Furaha kama kifo humtokea mtu Yeyote hata awe mfamle au nabii wote watakufa Tu.